01.10.08 - ICTR/AMOUSSOUGA - MSEMAJI WA ICTR ASAFISHWA KWA KUKIUKA TARATIBU ZA KAZI

Arusha, Oktoba 01, 2008 (FH) - Kamati ya Pamoja Inayoshughulikia Nidhamu katika Umoja wa Mataifa (JDC) imemfutia madai ya ukiukwaji wa taratibu za utendaji kazi yaliyokuwa yanamkabili Msemaji wa Mahakama ya Kimtaifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR), Roland Amossouga ambayo yalisabisha kuondolewa kwa muda katika nafasi yake na kupangiwa kazi nyingine Oktoba 2005.

0 min 58Approximate reading time

Kamati hiyo iliundwa kufuatia madai kwamba Amoussouga alimsaidia kinyume cha taratibu, Wakili mmoja raia wa Ufaransa, Pascal Besnier apate kazi ya Mkuu wa Mawakili wa Utetezi na Kitengo cha Uongozi wa Gereza la ICTR.

Kamati iliyokuwa inachunguza suala hilo dhidi ya Amossouga sasa imeachana na hoja hiyo na kumsafisha Amoussouga dhidi ya madai hayo. Naye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon alikubalina moja kwa moja na maamuzi hayo na kuyapitisha Septemba 15, mwaka huu.

"Baada ya kuchambua kwa makini madai hayo, Kamati ya Nidhamu kwa kauli moja imependekeza kuachana na madai hayo na hakutakuwa na hatua nyingine ya kidhamu itakayochukuliwa," sehemu ya sekula iliyotolewa Septemba 30, 2008 na Mkuu wa Kitendo cha Utawala ICTR, Sarah Kilemi imeeleza.

Awali kufuatia madai hayo Msajili wa Mahakama hiyo alichukua hatua za haraka kusitisha ajira hiyo na kumsimamisha kwa muda Amoussouga kuwa Msemaji wake.Hata hivyo alirudishwa katika nafasi hiyo Juni mwaka jana.

Kutokana na matokeo hayo ya uchunguzi, Kilemi alisema baadhi ya hatua za dharura zilizochukuliwa Oktoba 6, 2005 ambazo bado zinatekekelezwa "zitaangaliwa upya."

Alipoulizwa juu ya suala hilo, Amoussouga mwenyewe hakutaka kutoa maoni mengi zaidi ya kusema " nimepata ahueni kwamba sasa jambo hilo limehitimishwa."

Wakili Besnier hakupatikana kutoa maoni yake.

SC/NI

© Hirondelle News Agency